Utafiti wa TADIP Urais 2015 Wampa Lowassa ushindi kwa 54.5% dhidi ya Magufuli (40%)


Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Tanzania Development Initiatives  Program (Tadip), iliyofanya utafiti wa “Kuelekea Uchaguzi Mkuu  Watanzania wanasemaje” imeonyesha mgombea wa Chama cha Demokrasia na  Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, anaongoza kwa asilimia 54.4 na  mgombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli akifuatia kwa  asilimia 40.

Utafiti huo umekuja siku chache tu baada ya awali uliotolewa na  Taasisi ya Twaweza kuonyesha Dk. Magufuli anaongoza kwa asilimia 65  na Lowassa akipata asilimia 25.

Katika utafiti uliotolewa juzi na Umoja wa Katiba ya Wananchi  (Ukawa), ulionyesha Lowassa ana asilimia 76 ya watu wanaomuunga mkono.
 
Kwa upande wa wagombea urais wa vyama vingine vya siasa Tadip ilisema  mgombea wa ACT-Wazalendo, Anna Mghwira amepata asilimia mbili,  akifuatiwa na mgombea wa Chaumma, Hashim Rungwe, alipata asilimia  0.4,  huku mgombea wa ADC, Chief Yemba akipata asilimia 0.1 na  asilimia tatu ya wananchi walisema hawafahamu wanampa nani kura.

Mkurugenzi wa Tadip, George Shumbusho, akizungumza na waandishi wa  habari jana jijini Dar es Salaam kuhusu utafiti huo, alisema  ulifanyika kuanzia Septemba 4 -23, mwaka huu.

“Utafiti huu uliwalenga wananchi moja kwa moja ambao waliojiandikisha  kwenye daftari la kudumu la wapiga kura kwa kutumia mfumo wa  Biometric Voter Registation (BVR). Ulifanyika kwa wiki tatu za mwezi  huu na mikoa tuliyolenga ni ile ambayo Tume ya Taifa ya Uchaguzi  (Nec) ilithibitisha kuwa ina idadi kubwa ya watu,” alisema Shumbusho.

Aidha, utafiti huo ambao ulilenga mikoa 12, ulionyesha kuwa, Lowassa  anaungwa mkono na wanaume ambao ni asilimia 57 ya waliotoa maoni huku  Dk. Magufuli na Anna Mughwira wakiungwa na wanawake kwa asilimia 43  ya waliopiga kura.

Kuhusu idadi ya walioshiriki katika utafiti huo, alisema walitumia  njia za madodoso kuwapa wananchi 2,500 ambao kati yao 2,040 ndio  waliorudisha madodoso.

“Tulitumia njia ya kuwapa watu wetu madodoso ambayo waliyafikisha kwa  wananchi kati ya nyumba 20 walitoa kwa mtu mmoja na walioweza kujibu  madodoso ni 2,040. Tulipokea pia ripoti ya mdodoso na mdodoswa,”  alisema. 
 
Alitaja mikoa waliyojikita katika utafiti huo kuwa ni Dar es  Salaam, Mbeya, Mwanza, Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Shinyanga, Geita,  Dodoma, Morogoro, Kagera na Kigoma.


Alisema katika ya mikoa hiyo mikoa ya Kagera na Kigoma ilishindwa  kupata maoni yao kutokana na kuwahi ukomo wa kuwasilisha takwimu hizo  kwa wananchi.
Share on Google Plus

    Blogger Comment