Sumatra Yafungia Mabasi yote ya Muro


MAMLAKA ya Kudhibiti Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), imesitisha kwa muda usiojulikana leseni ya usafirishaji abiria ya kampuni ya mabasi ya Muro (Muro Investment Co. Limited), kwa kutokidhi viwango vya kiufundi na usalama.

Aidha, Sumatra imeiagiza kampuni hiyo kuwasilisha kwa mamlaka hiyo mpango wa utengenezaji magari yake, nakala ya cheti cha ofisa usafirishaji wa kampuni pamoja na mkataba wake wa ajira, iweze kujiridhisha endapo matakwa ya kanuni za ufundi, ubora na usalama yamezingatiwa na kutimizwa.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Gilliard Ngewe, kampuni hiyo ilijulishwa kuhusu uamuzi huo ambao utekelezaji wake unaanza leo kwa mabasi yote ya Muro yanayosafirisha abiria kutoka Dar es Salaam- Arusha na Dar es Salaam- Mwanza.

Kufuatia maelezo ya Ngewe, mabasi hayo yamekuwa yakilalamikiwa na abiria kwa kuharibika mara kwa mara pindi yawapo safarini, hivyo kushindwa kutoa huduma ya usafiri kwa viwango vinavyotakiwa.

Alisema, “Inapotokea mabasi yanayosafirisha abiria yanapata hitilafu za mara kwa mara na kushindwa kuwapa abiria mabasi mbadala wakamilishe safari zao, mamlaka inawajibika kufanya uchunguzi na kuchukua hatua stahiki, ikiwa ni pamoja na kusitisha leseni ya usafiri kwa kampuni husika”.

Mkurugenzi Mkuu huyo alisema, hatua iliyochukuliwa dhidi ya kampuni ya Muro ilizingatia ushahidi uliotolewa na abiria waliofikisha malalamiko yao kwa mamlaka hiyo, wakiwemo walioachwa wakihangaika njiani Septemba 17, mwaka huu, kwa zaidi ya saa 15 bila kupatiwa suluhisho wala huduma za kibinadamu.

Inaelezwa abiria hao walikuwa wakisafiri kwa basi la Muro lenye namba za usaji T51BQP, kutoka Dar es Salaam kwenda Arusha, lililoharibika katika eneo la Chalinze mkoani Pwani saa 3:00 asubuhi hadi saa 6:30 usiku, bila wahusika kuwaeleza abiria chochote.

Mamlaka hiyo pia ilieleza kuwa, abiria wa mabasi hayo yaendayo Mwanza yakitokea Dar es Salaam wamekuwa wakikutwa na kadhia ya aina hiyo wawapo safarini, ambapo mara kwa mara wamejikuta wakihangaika njiani pindi yanapoharibika bila kupatiwa ufumbuzi wa haraka.

Ngewe alitaja mabasi mengine ambayo yanahusika na adhabu hiyo kuwa ni lenye namba za usajili T780BPY lililoharibika Septemba 5, mwaka huu katika eneo la Ruvu Darajani mkoani Pwani na T788BPY lililoharibika Septemba 11, mwaka huu katika eneo la Mailimoja-Kibaha mkoani humo.

Mabasi mengine yaliyofungiwa ni yenye namba za usajili; T 881 BUR, T 485 BQV, T 536 CYC, T 540 CYC, T 534 CYC, T 531 CYC.

 “Makosa yaliyofanywa na kampuni ya Muro ni ukiukwaji wa kanuni namba 21 na 22 ya Kanuni za Leseni za usafirishaji kwa magari ya abiria ya mwaka 2007 na Kanuni namba 11 ya (1)(b) ya viwango vya ubora na usalama vya mwaka 2008,” alisema.

Sumatra ilieleza kuwa kufunguliwa kwa leseni kwa kampuni hiyo kutategemea majibu yatakayotolewa na mkaguzi wa magari kutoka jeshi la Polisi, baada ya matengenezo yatakayofanywa katika magari hayo.
Share on Google Plus

    Blogger Comment