Askari Wakamatwa kwa Kumuua Mdhamini wa Mtuhumiwa kesi ya Wizi wa fedha kwa Mtandao


Polisi mkoani Mbeya inamshikilia Mkuu wa kituo kidogo cha Polisi Ikata mkoani humo, Steven Rajab pamoja na askari mgambo wawili waliofahamika kwa jina moja moja, Labani na Kafurafumbi, kwa kutuhumiwa kumpiga Simioni Mndolwa na kusababisha kifo chake siku nne baadaye.

Kamanda wa Polisi Mbeya, Ahmed Msangi amesema kuwa watuhumiwa wanashikiliwa kwa mahojiano huku kituo hicho kikiwa kimefungwa hadi hapo watakapopelekwa askari wengine.

Imeeelezwa na ndugu wa marehemu pamoja na mwenyekiti wa kijiji kuwa, marehemu alifikwa na mauti kutokana na majeraha aliyoyapata alipopigwa kutokana na kutokuonekana kwa Nebati Nkwale, anayekabiliwa na kesi ya wizi wa fedha kwa njia ya mtandao ambaye marehemu alikuwa amemdhamini. Nkwale alitokomea kusikofahamika baada ya kupewa dhamana.

Mke na watoto wa marehemu wameripoti kuwa walifika mara kadhaa kituoni hapo wakiomba kuondoka na Mndolwa wakati akiwa bado hai ili atibiwe lakini hawakuruhusiwa hadi watoe dhamana ya shilingi laki tano


Mke wa marehemu ameeleza kuwa walilazimika kuuza ng’ombe ili kupata kiasi cha fedha kilichotawa. 
 
Baada ya kufanikiwa kumpatia dhamana na kufanikiwa kumfikisha nyumbani, hali ya mgonjwa ilikuwa dhoofu kiasi cha kushindwa kuzungumza. 
 
Alipelekwa hospitali ya Mbozi Mission ambapo aliandikiwa rufaa na kwenda hospitalini Mtwara ambapo alikata roho akiwa katika chumba cha mapokezi.
Share on Google Plus

    Blogger Comment